Thursday 14 March 2013

WATANZANIA WAASWA KUNYWA MAJI KWA WINGI

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewahimiza Watanzania kuwa na tabia ya kunywa maji mengi kila siku ili kujikinga na matatizo ya figo ambayo yanazidi kuongezeka kila siku. Ametoa wito huo leo mchana (Alhamisi, Machi 14, 2013) wakati akizungumza na mamia ya wananchi wa mji wa Arusha waliohudhuria kilele cha maadhimisho ya Siku ya Afya ya Figo Duniani yaliyofanyika kwenye viwanja vya hospitali ya AICC jijini humo. Kaulimbiu ya Siku ya Afya ya Figo Duniani mwaka huu ni “Figo Salama kwa Maisha yako: Epusha Madhara Makubwa kwa Figo” au “Kidneys for Life: Stop Acute Kidney Injury”. Waziri Mkuu
alisema mtoto wa miaka 10 hadi mtu mzima wanatakiwa wanywe maji kiasi kisichopungua lita moja na nusu kwa siku wakati mtoto mwenye mwaka mmoja anatakiwa anywe maji yasiyopungua nusu kikombe (sawa na mililita 100) na kwamba kiasi hicho huongezeka kadri umri wa mtoto unavyoengezeka. “Hii itasaidia kuhakikisha hawaishiwi maji mwilini,” aliongeza.
Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, imekadiriwa kuwa watu milioni mbili hupoteza maisha kila mwaka kutokana na maradhi ya ghafla ya figo wakati asilimia 20 ya vifo vya wagonjwa waliolazwa hospitalini husababishwa na maradhi hayo.
“Wataalam wanasema maambukizi ya magonjwa hayo husababisha madhara makubwa ya figo (Acute Kidney Injuries) ambayo huchangia kwa kiasi kikubwa kuharibika kwa utendaji kazi wa figo. Hali hiyo husababisha watu kupata ugonjwa wa ghafla wa figo (mshtuko wa figo) na pia kusababisha athari kubwa kwenye figo na kuzifanya zishindwe kufanya kazi ipasavyo,” alisema.
Alisema maradhi yanayoweza kujitokeza ghafla na kuharibu figo hayajatiliwa mkazo ipasavyo, hasa katika nyanja za utoaji mafunzo ya tiba, utafiti na elimu ya afya ya figo kwa umma. “Hali hii husababisha kutotumika kikamilifu kwa fursa za kubaini maradhi yanayojitokeza ghafla na kuharibu figo; pia inaathiri utoaji huduma za afya ya figo usiokidhi, na hivyo wagonjwa kulazwa kwa muda mrefu hospitalini,” alisititiza.
Chanzo: MjengwaBlog

No comments:

Post a Comment