Thursday 30 May 2013

MAPENDEKEZO YA KAMATI YA MARIDHIANO ZANZIBAR KUHUSU UPI UWE MWELEKEO WA WAZANZIBARI

MAPENDEKEZO YA KAMATI YA MARIDHIANO ZANZIBAR KUHUSU UPI UWE MWELEKEO WA WAZANZIBARI KATIKA KUIJADILI RASIMU YA KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA ITAKAYOTOLEWA NA TUME YA MABADILIKO YA KATIBA
UTANGULIZI:
… Baada ya wananchi wa Zanzibar kutoa maoni yao juu ya vipi Muungano wa Zanzibar na Tanganyika unapaswa kuwa, hatimaye Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatarajiwa kutoa rasimu ya awali ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kati ya mwishoni mwa mwezi Mei na mwanzoni mwa mwezi Juni 2013.
Wakati tunaisubiri kwa hamu rasimu hiyo itolewe na kujua kilichomo, sisi wajumbe wa Kamati ya Maridhiano Zanzibar tumekaa na kutafakari juu ya upi unapaswa kuwa mwelekeo wa Wazanzibari katika kuijadili rasimu hiyo pale itakapotoka.
Baada ya mashauriano ya kina kati ya wajumbe wa Kamati ya Maridhiano na pia kwa kuwahusisha watu wengine mashuhuri hapa Zanzibar, tumekuja na mapendekezo yafuatayo ambayo leo hii tunayawasilisha kwa wananchi wa Zanzibar kupitia Kongamano hili. Haya si maagizo bali ni mashauri yenu na pindi mkiyakubali basi tutakuombeni tuyafanyie kazi kwa pamoja kwa kuyatumia katika kuipokea na kujadili rasimu pale itakapotolewa.
Mapendekezo yetu ni kama ifuatavyo:
1. Jina la Muungano:
Muungano huu umetokana na Jamhuri mbili kuungana kwa hiyari. Jamhuri hizo ni Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika. Jina la awali lililotajwa katika Mkataba wa Muungano la muungano wa jamhuri hizi mbili lilikuwa ni Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Jina hili baadaye mwezi Oktoba 1964 lilibadilishwa na kuitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ukiangalia mifano ya nchi nyingine zilizoungana, jina la muungano huweka bayana kwamba zilizoungana ni zaidi ya nchi moja, zaidi ya falme moja au zaidi ya jamhuri moja. Kwa mfano, muungano wa nchi (states) za Marekani unaitwa kwa kiingereza United States of America (USA), ule uliokuwa muungano wa jamhuri za kisovieti ukiitwa Union of Soviet Socialist Republics (USSR) na ule muungano wa falme za kiarabu unaitwa United Arab Emirates (UAE).
Ili kuondosha dhana iliyojengeka kwamba muungano wa jamhuri zetu mbili umeunda nchi moja na kuzifuta nchi zetu, Katiba Mpya inapaswa kuweka jina linalotambua msingi huo na historia hiyo. Hivyo basi, jina jipya liwe ni Muungano wa Jamhuri za Tanzania na kwa kiingereza United Republics of Tanzania.
Jina hili litasaidia utambulisho wa nchi wanachama katika uwanja wa kimataifa pale litapoambatanishwa katika nyaraka zote rasmi pamoja na jina la nchi husika. Kwa maana hiyo katika uwanja wa kimataifa na katika pasi za kusafiria utaweka wazi na kuwa na “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – REPUBLIC OF ZANZIBAR” na “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – REPUBLIC OF TANGANYIKA”.
2. Mipaka ya Zanzibar na Tanganyika:
Wakati zinaungana, Zanzibar na Tanganyika zilikuwa tayari ni nchi zenye mamlaka kamili zikiwa ni wanachama wa Umoja wa Mataifa na hivyo kila moja ilikuwa na mipaka yake inayoeleweka. Katiba na sheria za nchi mbili hizi ziliweka bayana mipaka hiyo na mipaka hiyo ilitambuliwa chini ya sheria za kimataifa.
Rasimu ya Katiba Mpya ni lazima itamke kwa uwazi kabisa na kutambua na kuheshimu mipaka ya nchi mbili hizi kama ilivyokuwa kabla ya siku ya Muungano tarehe 26 Aprili, 1964.
Baada ya hapo, Katiba ya Zanzibar na Katiba ya Tanganyika (itakayotungwa baada ya kupata Katiba mpya ya Muungano) kila moja iweke wazi mipaka yake.
3. Uraia:
Uraia ndiyo msingi wa ujananchi. Kwa vyovyote vile Katiba Mpya isijumuishe suala la Uraia kuwa la pamoja kupitia Muungano. Kila nchi mwanachama katika muungano ibakie na uraia wake na iratibu masuala yote yanayohusu uraia wake na raia zake. Kwa kufuata mfano kama wa Muungano wa Ulaya (European Union), unaweza kuwa na haki inayotambulika kikatiba ya uhuru wa raia wa nchi moja mwanachama kwenda katika nchi nyengine mwanachama kupitia utaratibu maalum utakaowekwa (free movement of people). Hata hivyo, kila nchi mwanachama iwe na haki ya kuweka utaratibu wa vipi raia hao watafaidi haki na fursa za nchi mwanachama nyingine.
Hili ni la muhimu hasa kwa nchi ndogo kama Zanzibar ambayo ina rasilimali ndogo ya ardhi na hasa ikizingatiwa kuwa ardhi ilikuwa mojawapo ya sababu kuu za kufanyika Mapinduzi. Katika hali kama hiyo, Zanzibar ina sababu nzito za kuona inadhibiti na kusimamia wenyewe Uraia wake na utambulisho wa raia hao.
Hivyo basi, suala la Uraia lisiwemo katika mambo ya Muungano na badala yake kila nchi isimamie yenyewe masuala ya Uraia.
Hata hivyo, kunaweza kukawepo chombo cha pamoja kinachojumuisha nchi mbili hizi cha kuratibu masuala ya Uraia na haki na fursa ambazo raia wanaweza kuwa nazo kwa kila upande.
4. Uhamiaji:
Kutokana na sababu tulizozitaja hapo juu kuhusiana na suala la Uraia inapelekea wazi kuwa kila nchi mwanachama idhibiti na kusimamia wenyewe mambo ya Uhamiaji. Hivyo basi, rasimu ya Katiba Mpya isijumuishe suala la Uhamiaji kuwa ni suala la Muungano.
Kila nchi mwanachama kati ya Zanzibar na Tanganyika iwe na paspoti yake yenyewe yenye kubeba jina la nchi yake na nembo yake ya Taifa na yenye kudhamini usalama wa raia wake nje ya nchi kupitia uhakikisho unaotolewa na Serikali ya nchi husika.
Ili kuonesha sura ya kuwepo muungano wa kisiasa, paspoti za nchi mbili hizo zinaweza kuwa na jina la Muungano juu na kufuatiwa na jina la nchi mwanachama likiambatana na nembo ya Taifa ya nchi hiyo. Kwa mfano, “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – ZANZIBAR PASSPORT” na “UNITED REPUBLICS OF TANZANIA – TANGANYIKA PASSPORT”.
Kwa upande mwengine kunaweza kukawa na mamlaka ya kuratibu masuala ya uhamiaji wa nchi hizi mbili (Union immigration regulatory authority) kwa lengo la kuweka na kuratibu mfumo mzuri wa mawasiliano kati ya mamlaka za uhamiaji za nchi mbili hizi.
5. Mambo ya Nje:
Mamlaka juu ya mambo ya nje na uwezo wa nchi kuingia mikataba na nchi nyingine na mashirika ya kimataifa ndiyo roho ya nchi yoyote duniani kutambulika kimataifa na kuweza kusimamia mamlaka yake ya ndani yanapohitaji mashirikiano na nchi nyengine.
Ili nchi iweze kutambulika kimataifa inapaswa kuwa na mambo manne yafuatayo:
(a) eneo la ardhi lenye mipaka inayotambulika;
(b) watu wanaoishi kwenye eneo hilo wanaojitambulisha na eneo hilo;
(c) serikali inayotekeleza majukumu yake; na
(d) uwezo wa kuingia katika mahusiano ya kimataifa na nchi nyengine.
Kwa msingi huo, Wazanzibari wanahitaji kuona kuwa Mambo ya Nje haijumuishwi katika orodha ya mambo ya Muungano na badala yake kila nchi isimamie yenyewe mamlaka yake juu ya mambo ya nje.
Hata hivyo, uratibu wa sera ya mambo ya nje (foreign policy coordination) inaweza kuwa ni suala la muungano lakini utekelezaji wake kila nchi ikausimamia kupitia Wizara yake ya Mambo ya Nje. Uratibu wa sera ya mambo ya nje unaweza kufanywa kupitia chombo cha pamoja kitakachoundwa na Wizara za Mambo ya Nje za nchi mbili hizi kwa mfano kuwa na Council on Foreign Policy.
Kutokana na hoja hizo hapo juu inabaki kuwa kila nchi iwe na uanachama na kiti chake katika Umoja wa Mataifa na jumuiya nyengine za kimataifa. Hayo si ajabu katika miungano. Umoja wa Jamhuri za Kisoshalisti za Kisovieti (USSR) ulikuwa na uanachama na kiti chake Umoja wa Mataifa lakini miongoni mwa nchi wanachama, Jamhuri tatu za Ukraine, Belarus na Georgia ziliamua kuwa na uanachama na viti vyao katika Umoja wa Mataifa na hilo liliwezekana.
Kwa msingi huo huo, Zanzibar iwe na uanchama wake katika Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Madola, Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya SADC na jumuiya nyengine za kikanda na za kimataifa.
6. Sarafu, Benki Kuu, Mikopo na Biashara ya Nchi za Nje, Ushuru wa Forodha, Kodi ya Mapato na Kodi ya Mashirika:
Uchumi si suala la Muungano hata katika Katiba inayotumika sasa. Hata hivyo, nyenzo za kuendeshea na kusimamia uchumi wa nchi kwa maana ya sera za fedha na uchumi (fiscal and monetary policies) zimeendelea kudhibitiwa kupitia Serikali ya Muungano.
Vyombo vikuu vinavyosimamia sera hizo ambavyo ni Benki Kuu (BOT), Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA) na Wizara ya Fedha ya Serikali ya Muungano vimekuwa vikifanya maamuzi na kuyatekeleza bila ya kuzingatia kuwa kwa maumbile uchumi wa Zanzibar ambao ni uchumi unaotegemea utoaji wa huduma (service oriented economy) hauwezi kuwa sawa na uchumi wa Tanganyika ambao unategemea rasilimali (resource based economy). Sera za fedha na uchumi zikiwemo zile zinazohusu udhibiti wa sarafu na viwango vya kodi, ushuru na riba katika mabenki zimekuwa zikitungwa bila ya kuzingatia msingi huo wa chumi mbili zilizo tofauti na badala yake mara zote zimeegemezwa kwenye kulinda maslahi ya uchumi wa Tanganyika.
Sarafu ya pamoja imekuwa ikishuka thamani kwa kasi kila uchao kutokana na sababu nyingi lakini miongoni mwake zaidi zinatokana na uendeshaji mbaya wa uchumi wa Tanganyika. Serikali inapochapisha sarafu zaidi ili kudhibiti mfumko wa bei athari zake zinaikumba pia Zanzibar.
Zanzibar inahitaji kujikomboa kiuchumi ili iweze kutekeleza malengo ya Mapinduzi kwa wananchi wake na hivyo inahitaji kuwa na mamlaka yake kamili katika kusimamia masuala ya sera za fedha na uchumi yakiwemo masuala yote yanayohusu sarafu, viwango vya kodi na ushuru pamoja na riba katika mabenki, mikopo na biashara ya nchi za nje.
Kutokana na hali hiyo, masuala ya sarafu, benki kuu, mikopo na biashara ya nchi za nje, ushuru wa forodha, kodi ya mapato na kodi ya mashirika kila nchi inapaswa iyasimamie yenyewe.
7. Polisi:
Pamoja na kuwemo katika mambo ya awali ya Muungano lakini uendeshaji wa Polisi umekuwa na matatizo yake katika muungano. Miaka yote Polisi Zanzibar imekuwa ikilalamika kuwa inachukuliwa kama vile ni Mkoa tu na hata bajeti na mahitaji yake mengine yanachukuliwa hivyo hivyo na makao makuu ya Polisi yaliyopo Dar es Salaam.
Katika nchi nyingi duniani Polisi ambayo inashughulika na usalama wa raia na mali zao imekuwa ikiendeshwa chini ya Serikali za Manispaa na hata Majimbo seuze kwa nchi kama ilivyo Zanzibar.
Ukiondoa mishahara na bajeti ndogo ya uendeshaji inayotolewa na makao makuu ya Polisi, gharama nyengine za uendeshaji wa polisi kwa Zanzibar zimekuwa zikichangiwa na mamlaka za Zanzibar ikiwemo Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB).
Hivyo basi, wakati umefika kuona mamlaka kuhusu Polisi yanaondolewa katika orodha ya mambo ya Muungano na kila nchi ishughulikie yenyewe Polisi yake.
8. Mafuta na Gesi Asilia (pamoja na maliasili nyengine zote):
Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kwa niaba ya Wazanzibari lilishafanya maamuzi mwezi Aprili 2009 kuyaondoa masuala ya mafuta na gesi asilia kutoka kwenye orodha ya mambo ya Muungano. Mbali na maazimio ya Baraza la Wawakilishi, masuala ya mafuta na gesi asilia yanahusu uchumi ambalo si suala la Muungano.
Katiba Mpya haipaswi kuyajumuisha masuala hayo mawili (pamoja na maliasili nyengine kwa ujumla) kuwa mambo ya Muungano.
Hivyo basi, rasimu yoyote itakayoyajumuisha masuala hayo ya Mafuta na Gesi Asilia (pamoja na maliasili nyengine zote kwa ujumla) kuwa masuala ya Muungano haitakubalika kwa Wazanzibari.
9. Vyama vya Siasa:
Muungano uliundwa na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika kupitia serikali zao. Mazungumzo yaliyopelekea muungano huo na hata utekelezaji wa hatua za kuunganisha nchi mbili hizi katika muungano hayakuhusisha vyama vya siasa vya wakati huo, ASP kwa upande wa Zanzibar na TANU kwa upande wa Tanganyika. Ndiyo maana kwa miaka 13 ya Muungano (kuanzia 1964 hadi 1977) kila nchi kati ya nchi mbili hizi iliendelea kuongozwa na chama chake cha siasa.
Moja kati ya dhoruba kubwa dhidi ya makubaliano ya asili ya muungano huu ambayo ni Mkataba wa Muungano ilikuwa ni kuunganisha vyama vya siasa vya ASP na TANU na kuunda CCM ambacho kilijitangazia kushika hatamu na kuwa juu ya vyombo vyengine vyote vya nchi zikiwemo Serikali. Utaratibu huo uliingizwa ndani ya Katiba za nchi na hivyo kuuhalalisha kisheria. Tokea wakati huo, Zanzibar imekosa mamlaka ya kisiasa ya kufanya maamuzi yake kwa mambo yanayoihusu. Na pale ilipofanya hivyo ilifanya kwa kutegemea na kujiamini kwa uongozi uliopo Zanzibar ingawa majaribio ya kutumia nguvu ya vyama kuzuia maamuzi kama hayo yamekuwa yakifanyika na baadhi ya wakati kufuzu.
Maongozi ya nchi yoyote yanategemea historia, mila na utamaduni wa watu wa nchi husika.
Kwa msingi huo basi, na ili Zanzibar iweze kurejesha mamlaka yake ya kisiasa katika kufanya na kusimamia maamuzi kwa mambo yake, rasimu ya Katiba haipaswi kujumuisha suala la vyama vya siasa kuwa ni jambo la Muungano. Zanzibar na Tanganyika kila moja iweze kuandikisha vyama vyake vya siasa.
10. Utaratibu wa uendeshaji wa Mambo ya Muungano:
Kwa yale mambo yatakayokubaliwa kubaki katika Muungano kama vile:
- Katiba ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania;
- Serikali ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania;
- Uratibu wa Sera ya Mambo ya Nje;
- Ulinzi;
- Usalama;
- Mamlaka juu ya mambo yanayohusika na hali ya hatari;
- Utumishi katika Serikali ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania; na
- Mahkama ya Rufani ya Muungano wa Jamhuri za Tanzania.
Utaratibu wa uendeshaji wake uwekwe wazi katika Katiba kwamba maamuzi yote yatafanywa kwa mashauriano na makubaliano kati ya nchi mbili zinazounda Muungano huu na yatakuwa halali tu iwapo yatafuata msingi huu.
HITIMISHO:
Haya kimsingi ndiyo mapendekezo yetu Kamati ya Maridhiano. Tunayaleta kwenu muyapokee, muyajadili na kuwaomba muyaridhie ili yawe ndiyo msingi wa mwelekeo wa wananchi wa Zanzibar ambao wengi wao waliojitokeza mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba walitaka nchi yao iwe na mamlaka kamili.
Kwa mapendekezo haya, tunadhani Zanzibar na Tanganyika zitaendelea kuwa na mashirikiano ya kidugu kupitia mfumo mpya wa Muungano na wakati huo huo kila nchi mwanachama wa muungano ikibaki na mamlaka yake kamili katika yake maeneo ya msingi ambayo kila nchi hupenda kuwa nayo.
Imetolewa:
Zanzibar
25 Mei, 2013
Source: Jussa’s Wall on facebook

No comments:

Post a Comment