Thursday 25 July 2013

Wanasiasa Z’bar na propaganda dhaifu

Leo nalazimika kuandika makala haya kwa mshangao mkubwa wa baadhi ya wanasiasa hapa Zanzibar kutengeneza taswira ambayo haikubaliki wala kuendana na wakati tulionao.
Kuna baadhi ya wanasiasa wanatumia propaganda dhaifu kwamba wanaodai mabadiliko katika muundo wa Muungano wanataka kumrejesha Sultan!
Hii ni ajabu ya mwisho, pia ni aibu kusikia kauli kama hizo baada ya takriban miaka hamsini ya kujitawala.
Inafahamika vizuri kwamba Zanzibar ni nchi kamili na watu wake waliamua kujitawala wenyewe kupitia mapinduzi yaliyoung’oa utawala kisultan Januari 1964 na Aprili mwaka huu Jamhuri ya watu wa Zanzibar ikaungana  na Jamhuri ya Tanganyika kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 Sultan wa mwisho kutawala Zanzibar ni Jamshid bin Abdullah Al Said ambaye kwa sasa anaishi Portsmouth, Uingereza akiwa na umri wa miaka 83.
Hakuna anayemtambua katika medani za kisiasa kwa Zanzibar ya leo zaidi ya kubaki katika vitabu vya kihistoria tu, lakini kizazi hiki kinachojali ni nchi yao iliyo huru ambayo ilikombolewa kutoka kwa wakoloni.
Umezuka mtindo kwa wasiokuwa na nguvu ya hoja kudai eti kuna watu vibaraka wa Sultan, ndiyo maana wanadai mabadiliko katika Muungano!
Huu ni uzushi na uongo usiokuwa na hata chembe ya ukweli, wananchi wa Zanzibari chini ya Afro Shiraz Party ndio waliompindua Sultan na kuirejesha nchi yao mikononi mwa wazalendo ambao ni wakwezi na wakulima; iweje leo miaka 49 tukijiandaa kuadhimisha jubilee ya miaka 50 ya Mapinduzi watamani kutawaliwa tena?
Kama leo itapigwa kura, kuulizwa nani kati ya Abeid Amani Karume na Sultan Jamshid anayefahamika, jawabu lisilokuwa na hata chembe ya shaka ni Karume. Sultan hana mlango wa kuingilia Zanzibar.
Kabla ya Mapinduzi, Zanzibar haikuwa Jamhuri, ilikuwa chini ya Sultan, lakini Mapinduzi ya umma ndio yaliyoifanya Zanzibar kuwa Jamhuri.
Umoja wa Mataifa uliyatambua Mapinduzi hayo kuwa ni halali na uliokuwa Umoja wa nchi huru za Afrika (OAU) uliyatambua pia.
Sheria na mikataba ya kimataifa haitoi nafasi kwa Sultan kujipenyeza Zanzibar na wala hicho kiti chake huko UN hakipo, kilibiruka mwaka 1964. Kwa hiyo msipoteze muda kwa propaganda mfu na zisizokuwa na mashiko.
Vuguvugu la mabadiliko lililoanzia na Mapinduzi ya kule Ufaransa yaliamsha ari na kuwatia shime wazalendo wa Zanzibar kufanya Mapinduzi yaliyosimamiwa na kuratibiwa na ASP.
Athari za Mapinduzi ya Ufaransa zilienea kote duniani na ilipofika Januari 12, 1964, Wazalendo wa Zanzibar chini ya Afro Shiraz Party walirejesha heshima na utu kwa wakulima na wakwezi.
Wazanzibari sasa wanataka mabadiliko, hawatafanya kama wale wa Ufaransa isipokuwa watatumia haki ya kutoa mawazo yao, iwe wanataka Serikali tatu au mbili ni haki yao.
Saa ya mabadiliko imefika, vijana wasiokuwa na ajira, uhakika wa chakula wala kulala wamefikia pahala wanataka kuona mabadiliko ya kweli yanatokea siyo tu katika siasa bali hata katika uchumi na ndiyo maana wengi wanaunga mkono pendekezo la tume ya Jaji Warioba la kuwa na shirikisho.
Ni lazima wanasiasa wetu wafahamu kuwa ulimwengu wa leo, vijana haukubali tena kuburuzwa na mara nyingi vijana wa kileo waliozaliwa katika Teknohama wanaunga mkono siasa yenye uchumi na wanazuoni wanaipima hoja hiyo katika  mizania miwili; mosi, msukumo binafsi wa kijana wa Zanzibar wa uhitaji wa mabadiliko na pili, ni mhemko wa majira.
Mhemko huu ni kama kilevi ambapo kama ukweli ulivyo idadi kubwa ya vijana ndio wanywaji ambao hawatapenda kunywa kilevi kama togwa kisichokuwa na ‘stim’ yoyote kwao.
Demokrasia ya kisasa inalazimisha kuheshimu mawazo ya wengine hata kama huyataki, ndiyo maana watu makini wanaamini kuwa uvumilivu mzuri ni ule unaojiepusha na chuki zisizo na msingi (prejudice).
Hata kama anayetoa maoni au kueleza ni yule msiyeafikiana, au kimaumbile si mzungumzaji mzuri jaribu kuuweka sawa ujumbe wake kwa misingi ya nguvu ya hoja huku ukizingatia alichokizungumza siyo namna alivyozungumza. Mara zote chuki isiyo na msingi huviza mabadiliko.
Ikiwa dhana ya ujana ndio nguvu ya mabadiliko katika jamii, wanaobeza msimamo wa wale wanaotaka Serikali tatu, tumeona namna watu wa Zanzibar na Tanganyika walivyotoa mawazo yao kutaka mabadiliko ya msingi katika muundo wa Muungano.
 Watu wasijadili suala la muundo wa Muungano kwa jazba wala chuki kama ilivyoanza kujitokeza hivi karibuni kwa upande wa Tanganyika ambao wanawachukulia Wazanzibari kama wakorofi.
Hawa wanaokejeli wenzao tunawafahamu ndio masalia ya wanasiasa waliochoka kimawazo, wengine wana joto lao la kushindwa maisha na kukosa vyeo walipokuwa Serikalini, ndio leo wanamalizia hasira zao kwa wale wanaotoa hoja za kudai Muungano wenye usawa baina ya nchi ya Zanzibar na Tanganyika .
Haitawezekana kwa hali yoyote ile wananchi wa Zanzibar walio huru waliokataa kutawaliwa eti baada ya miaka 49 ya Mapinduzi watamani kutawaliwa tena na ukoloni wa Sultan!
Hili ni jambo la kushangaza kuona kwamba katika Afrika hii kuna watu wanamuota Sultan, napenda kuwaeleza kwamba Sultan na watu wake hawana hata chembe ya nafasi katika Zanzibar mpya, wala ya zamani.
Itakumbukwa pia kuwa mara tu baada ya Mapinduzi mwaka 1964, Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume kama ilivyo kwa Mwalimu Nyerere naye alichukia sana ubaguzi na ndio maana aliongoza kampeni ya ndoa za mchanganyiko wa rangi na makabila mbalimbali hapa Zanzibar.
Mzee Karume hakulazimisha watu kuoana bali aliwataka wazazi wawape watoto wao uhuru wa kuoa na kuolewa na wawapendao. Waarabu hawakutaka mabinti wao waolewe na Waafrika ilhali, na kinyume chake baadhi ya Waafrika walikataa watoto wao kuoa Waarabu.
Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment